SWALI NA. 1: Je maziwa yapi ni bora zaidi kwa mtoto wangu? Ni ya mama au ya kopo?
JIBU: Maziwa ya mama ni bora kuliko kitu kingine cho chote kwa
kuwa:
yana kinga za asili
yana virutubisho vyote
yanapatikana wakati wote hayahitaji kutayarishwa
ni safi na salama
yanamfaa mtoto mdogo
huleta uhusiano mzuri kati ya mtoto na mama yake
kunyonyesha kunasaidia kurudisha tumbo la uzazi la mama katika hali yake ya awali
katika miezi sita ya mwanzo mama anayenyonyesha mtoto wake kwa zaidi ya mara kumi kwa siku hapati siku zake za mwezi na hapati mimba mapema.
Maziwa ya kopo
siyo sawa na ya binadamu. Ni kazi kuyatayarisha na hayana virutubisho
kama maziwa ya mama. Ni chanzo cha magonjwa kama ya kuharisha.
MAZIWA YA MAMA NDIYO BORA KWA MTOTO WAKE
SWALI NA. 2: Je maziwa ya mama ya mwanzo ni
mazuri kwa mtoto?
JIBU: Ndiyo. Ni mazuri sana. Maziwa haya kwa lugha ya kizungu
yanaitwa Colostrum. Maziwa haya ni mazito, yenye rangi ya njano. Ni
muhimu mtoto anyonye maziwa haya kwani yamejaa kinga za asili
zitakazosaidia kumzuia mtoto asipate magonjwa hasa ya kuharisha na kifua.
SWALI NA. 3: Je mama mjamzito akishajifungua tu
mtoto wake ampe nini cha kumuonjesha hapa duniani, chumvi au sukari?
JIBU: Mama mjamzito anapojifungua tu, cha kumuonjesha mtoto wake
si chumvi wala sukari, bali ni maziwa yake mwenyewe. Maziwa ya mama yana
kila kitu, yaani chumvi na sukari humo humo. Ni safi, ni fresh, yana
usalama, yana viini vya kukinga mwili, yana joto linalomfaa mtoto na
hayamletei mtoto kuharisha. Zawadi kubwa ambayo mama anatakiwa kumpa
mtoto wake mchanga ni moja tu, nayo ni maziwa yanayotoka ndani ya ziwa
lake mwenyewe. Na ampe ziwa hilo kuanzia mara tu anapozaliwa mtoto.
Hakuna sababu yoyote ya kumchelewesha mtoto kunyonya ziwa.
SWALI NA. 4: Je mtoto anatakiwa aanze
kunyonyeshwa tangu lini? Mbona mimi maziwa yangu yalichelewa sana kuanza
kutoka na nikamwonea huruma mwanangu nikampa maji? Je nina upungufu gani
mwilini mwangu?
JIBU: Mtoto anatakiwa aanze kunyonyeshwa maziwa ya mama mara tu
anapozaliwa. Hakuna ulazima wowote wa kuchelewesha kitendo cha kumpa
mtoto ziwa la mama yake.
Maziwa yako yalichelewa kutoka kwa vile hukumpatia mtoto ziwa mara tu
alipozaliwa. Kitendo cha mtoto kunyonya huwa ndiyo msisimko kwa mama
kutoa maziwa. Hakuna haja ya kumpa mtoto maji, kwani yatamfanya mtoto
ajisikie kutosheka na hivyo asinyonye, na kutonyonya huko ndiko
kunakosababisha maziwa yasitoke. Narudia tena, wewe huna upungufu wowote
mwilini, ila huenda ulichelewa kumpa mtoto ziwa lako.
SWALI NA. 5: Je mtoto mdogo anayenyonya maziwa
ya mama tu anasikia kiu?
JIBU: Mtoto mdogo anayenyonya maziwa ya mama tu yaani mtoto aliye
na umri chini ya miezi 6 hahitaji maji ya kunywa. Maziwa ya mama yana
maji ya kutosha hata wakati wa joto kali. Mtoto mchanga hahitaji maji ya
kunywa mpaka afikishe miezi mine hata zaidi.
SWALI NA. 6: Je kuna utaalam maalum wa
kuwanyonyesha watoto wachanga?
JIBU: Hakuna utaalamu maalum wa kuwanyonyesha watoto wachanga,
kila mama anaweza kumnyonyesha mtoto wake. Hakikisha kuwa mtoto
anapatiwa ziwa la mama yake mara tu anapozaliwa. Pasiwe na kisingizio
cha mama kutokuwa na maziwa kwani kule kunyonyesha ndiko kunakomfanya
mama atoe maziwa. Mtoto anyonye mara nyingi kiasi atakachopenda mwenyewe,
asiwekewe vipimo. Hata wakati wa usiku mtoto asinyimwe kunyonya. Yote
hayo ni mambo yanayoweza kuzingatiwa na mama yeyote na hatuwezi kusema
kuwa yanahitaji utaalam maalum.
SWALI NA. 7: Mwanangu akinyonya maziwa yangu
anaharisha, Je maziwa yangu yameharibika? Kama yameharibika nifanye nini
ili yawe safi?
JIBU: Maziwa hayawezi kuharibika yakiwa ndani ya titi la mama.
Kama mtoto wako anaharisha labda kuna sababu nyingine lakini siyo maziwa
ya mama. Maziwa ya ng’ombe au ya kopo ndiyo yanayoweza kusababisha mtoto
kuharisha. Vile vile mtoto akiwa na ugonjwa kama vile malaria anaweza
kuharisha. Inafaa chanzo cha mtoto kuharisha kitafutwe kwa makini na
ikiwezekana ushauri upatikane kutoka kwenye kituo cha afya. Ni muhimu
ieleweke kwamba maziwa ya mama pekee hayamfanyi mtoto aharishe.
SWALI NA. 8: Kama mtoto wangu ananyonya vizuri,
ninatakia nianze lini kumpa vyakula vingine kwa mfano uji na kadhalika?
JIBU: Umri wa kumpa mtoto vyakula vingine, yaani vyakula vya
Kulikiza ni miezi minne. Kabla ya hapo mtoto awe ananyonyeshwa maziwa ya
mama tu. Mtoto akifikisha umri wa miezi minne azoeshwe vyakula vya
mchanganyiko, vilivyolainishwa kwa kiasi kidogo kidogo kwa muda wa miezi
ya kwanza. Afikapo miezi sita awe ameanza kula vyakula vya familia
vilivyopondwa pondwa, na taratibu kuongeza idadi ya milo kwa siku.
SWALI NA. 9: Nilipojifungua mtoto wangu wa
mwisho titi langu moja lilivimba sana. Majirani wakanishauri
nisimnyonyeshe mtoto wangu kutumia ziwa hilo. Nililiacha na kutumia titi
moja tu. Je ni sahihi?
JIBU: Siyo sahihi kuacha kumyonyesha mtoto titi lenye uvimbe.
Titi huvimba kama mtoto hakulinyonya vizuri na huendelea kuvimba
hatimaye kuwa na jipu kama mtoto hatanyonyeshwa. Njia ya kupunguza
uvimbe ni kuyakamua maziwa kwenye chombo ili kupunguza maziwa ndani ya
titi lililovimba na kuendelea kumnyonyesha mtoto katika titi hilo.
Uvimbe wa titi haudhuru maziwa ya mama na uvimbe hupungua haraka kama
mtoto ataendelea kunyonyeshwa.
SWALI NA. 10: Ninatakiwa niendelee kumnyonyesha
mtoto wangu mpaka awe na umri gani?
JIBU: Ili mtoto wako awe na afya nzuri unatakiwa uendelee
kumnyonyesha kwa muda wa miaka miwili au zaidi. Unashauriwa sana
usimwachishe ziwa mtoto wako kabla ya umri wa miaka miwili hata kama
amezoea vizuri chakula cha familia. Maziwa ya mama bado yana umuhimu
mkubwa katika umri huo.